Popular services

WANAWAKE WAISLAMU WAOMBWA KUIMARISHA DUA ZA KULIOMBEA TAIFA AMANI KUELEKEA UCHAGUZI MKUU 2025

 

NA FAUZIA MUSSA

MKE wa Rais wa Zanzibar, Mama Mariam Mwinyi, amewaomba wanawake Waislamu nchini kuendeleza ibada ya dua kwa ajili ya kuiombea nchi iendelee kubaki salama, yenye amani na utulivu, hasa katika kipindi hiki kinapokaribia uchaguzi mkuu wa mwaka 2025.

Akizungumza katika dua iloandaliwa na Kamati  Maalum ya dua ya kitaifa ya wanawake kwa kushirikiana na Ofisi ya Mufti Mkuu wa Zanzibar, iliyofanyika katika Masjid Mushawwal, Mwembe Shauri, Mama Mariam aliwashauri  wanawake waislamu wa Zanzibar kuendeleza juhudi hizo za dua na ibada ili nchi iendelee kuwa na amani ambayo ni msingi wa ustawi wa jamii.


" Kwa uwezo  wa Mwenyezi Mungu na ushirikiano wa wananchi wote, uchaguzi ujao utakuwa wa amani, wa haki na wa mafanikio kwa kila Mtanzania. Tunapaswa kumrudia Allah Mtukufu kwa unyenyekevu, tumuombe aendelee kutuwekea neema ya Amani kwani endapo amani itatoweka, wanawake na watoto ndio wahanga wakuu wa machafuko. Tumuombe Mola wetu kwa unyenyekevu ili uchaguzi uje na upite kwa salama, bila chuki, vurugu wala fitna.”

Aliongeza kuwa mafanikio na maendeleo ya Taifa hayawezi kupatikana bila ya amani na utulivu, na kwa hivyo ni wajibu wa kila Muislamu kushiriki katika maombi kwa makundi au mtu mmoja mmoja hata baada ya uchaguzi, ili Zanzibar, Tanzania na ulimwengu mzima udumu katika hali ya amani.

“Wenzetu wanaoishi katika nchi zenye migogoro na machafuko, hata mlo wa siku huwa ni mtihani. Hakuna kinachofanyika katika mazingira ya taharuki. Amani ni msingi wa ustawi na maendeleo ya jamii,” alisisitiza Mama Mariam.

Kiongozi wa dua hiyo, Maalim Sania, aliwashukuru wanawake waislamu na waumini wengine kwa kujitokeza kwa wingi na kuungana na viongozi wao katika ibada hiyo ya dua.

Alisema dua hiyo inalenga kumtaka Allah (Subhanahu wa Ta'ala) aijalie nchi amani, mshikamano na uongozi bora.

 “Dua ni silaha ya Muislamu. Tunapoomba kwa nia ya dhati, Allah hatushushi mikono mitupu. Tunamuomba Atupitishe salama katika uchaguzi, atuwekee viongozi waadilifu, wenye khofu ya Mwenyezi Mungu na walio tayari kuwatumikia wananchi kwa moyo wa uaminifu,” alisema Maalim Sania.

Alieleza kuwa dua hizo ni ishara ya dhamira ya Waislamu kuona taifa linapiga hatua kwa misingi ya amani, mshikamano na udugu na kuongeza  kuwa matumaini yao ni kuona Allah anazidi kuwakinga wananchi na hofu, fitna na vurugu, na badala yake kuzidisha mapenzi, umoja na mshikamano baina ya wananchi.

“Tumuombe Allah wakati wote, si tu kipindi cha uchaguzi, bali kila siku. Hakika dua ni ibada na ni mlango wa faraja kwa mwanadamu,” alisema maalim Sania

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Jumuiya mama  ya Wanawake Waislam wa Zanzibar, Hajjati Abla Sultan Mahmoud, alisema lengo kuu la dua hiyo ni kumuomba Allah awape uwezo wananchi kushiriki uchaguzi kwa salama, kwa uelewano na kwa moyo wa uzalendo.

“Tunawaomba wanawake wote Waislamu waendelee kuwa mstari wa mbele katika kuiombea nchi. Tushirikiane katika kuijenga jamii yenye maadili.” alisema Hajjati Abla.

Naye, Mjumbe wa Kamati ya Dua ya Kitaifa ya wanawake, Khadija Ali Hassan, aliwakumbusha wanawake nafasi yao ya kipekee katika kuhifadhi amani hasa kwa kulea vijana katika misingi ya dini na maadili mema.

“Wanawake tuendelee kuwa walinzi wa amani kupitia malezi ya vijana wetu. Historia inatufundisha kuwa vijana wasiolelewa vyema, ndio hutumiwa kama chombo cha kuvuruga utulivu wa taifa,” alisema Khadija.

Katika hafla hiyo, mamia ya wananchi kutoka mjini na vijijini walihudhuria, wakiongozwa na Mama Mariam Mwinyi pamoja na viongozi mbalimbali wa serikali, taasisi za dini na madrasa za Zanzibar.